Janga la COVID-19 likiendelea, mustakabali wa uhuru wa habari si mzuri. Hapa ni mambo kumi makuu

Waandishi wa habari waliovalia vifaa kinga wakisubiri karibu na majengo ambapo wakazi wanawekwa karantini kwa sababu ya ugonjwa wa COVID-19 mjini Kiev, Ukraine, mnamo Aprili 28, 2020. (Reuters/Gleb Garanich)

Na Katherine Jacobsen

Janga la ugonjwa wa COVID-19 limewapa kazi kubwa maafisa wa afya, limeathiri uchumi wa dunia, na kutumbukiza serikali kote duniani kwenye mzozo. Kadhalika, janga hili limeathiri jinsi wanahabari wanavyofanya kazi, miongoni mwa mengine kutokana na hali kwamba mamlaka katika mataifa mengi zimetumia ugonjwa huo kuminya uhuru wa vyombo vya habari.

Baadhi ya hatari zitafifia siku zinavyosonga: chanjo ya COVID-19 bila shaka itawakinga watu, wakiwemo waandishi wa habari, dhidi ya kueneza au kuambukizwa virusi hivi. Lakini baadhi ya hatua zilizowekwa zinazokandamiza uhuru wa wanahabari – ziwe za makusudi au zisizo za makusudi – huenda zikaendelea hata baadaye, wataalamu wanasema.

Kuna uwezekano kwamba hatua zilizochukuliwa kwa sababu ya virusi vya corona zitabadilisha kazi ya uanahabari kwa njia zisizoweza kutabirika, sawa na vile mashambulio ya Septemba 11, 2001, yalivyochochea sheria za kukabiliana na ugaidi kuenea duniani – na matokeo yake likasababisha ongezeko la visa vya wanahabari kufungwa, jambo linaloendelea hadi sasa..

Visa vya ukiukaji wa uhuru wa wanahabari duniani ambavyo CPJ imenakili kuhusiana na janga hili vinaweza kuwekwa kwenye makundi 10 ya kufuatiliwa kwa karibu (mifano imetolewa):

1. Sheria dhidi ya “taarifa za uzushi”

Janga hili limezipatia serikali kisingizio kipya cha kupitisha au kutekeleza sheria zinazoharamisha usambazaji wa “taarifa za uzushi,” “taarifa za kupotosha,” au “taarifa za uongo” – na kuzipa serikali sababu ya kutekeleza nyingine mpya. Katika kipindi cha miaka saba iliyopita, idadi ya wanahabari waliofungwa kwa makosa ya “taarifa za uzushi” au “taarifa za uongo” imeongezeka pakubwa, kwa mujibu wa utafiti wa CPJ..

Carlos Gaio, afisa wa kisheria wa ngazi ya juu nchini Uingereza anayefanya kazi na shirika la  Media Legal Defence Initiative, aliambia CPJ kwamba sheria za “taarifa za uzushi” zitaendelea kuenea serikali zikijaribu kudhibiti uenezaji wa habari kuhusu virusi hivi. Sheria hizo zitawaathiri wanahabari wa kawaida na wale wanaokabiliana na taarifa za uzushi bila kubagua. “Ni suala gumu kuharamisha kitu kama hicho [na ni] hatari sana,” Gaio alisema.

Taarifa za uzushi ni tatizo kubwa, lakini hatua hizi za kisheria zinazipa serikali uhuru wa kuamua ni habari gani zitaelezwa kuwa za uongo, jambo linalotoa ujumbe wa kuogofya kwa wanahabari wakosoaji wa serikali. Nchini Marekani, Rais Donald Trump mara kwa mara hukashifu ripoti za vyombo vya habari kuhusu COVID-19 na hutumia maneno ya kudhalilisha na kuwaita “taarifa za uzushi” anapotofautiana na ripoti hizo, mkakati ambao CPJ imebaini kwamba hufanikiwa katika kuvishusha hadhi vyombo ya habari na kupunguza imani ya umma kwenye vyombo hivyo. Desturi hii imekuwa kama ruhusa kwa watawala wa kiimla kuvidunisha na kuvihangaisha vyombo vya habari nchini mwao.

2. Kufungwa jela kwa wanahabari

Kukamatwa kwa wanahabari kumekuwa mbinu inayotumiwa na serikali za kiimla kwa kipindi kirefu kuzuia ripoti zinazokosoa serikali; takriban wanahabari 250 walikuwa jela kote duniani kwa mujibu wa hesabu ya mwisho ya CPJ ya kila mwaka iliyofanywa Desemba.  Wakati huu wa COVID-19, kufungwa jela kuna hatari kubwa; waandishi wanazuiliwa katika mazingira hatari kiafya na kulazimishwa kuwa karibu na watu wengine ambao wanaweza kuwa wameambukizwa. CPJ na mashirika mengine 190 kwa pamoja wametoa wito kwa watawala kote duniani kuwaachia huru wanahabari wote waliofungwa kwa sababu ya kutekeleza kazi yao.

Licha ya hayo, wanahabari bado wanakamatwa.

3. Kuzuia uhuru wa kujieleza

Baadhi ya hatua za dharura za serikali zimehusisha kubatilisha au kusimamisha haki ya uhusu wa kujieleza kipindi cha hali ya dharura.

4. Udhibiti wazi wa habari, mtandaoni na nje ya mtandao

Mamlaka katika mataifa kadha zimesitisha uchapishaji na usambazaji wa magazeti katika kile ambacho walisema ni juhudi za kudhibiti kusambaza kwa COVID-19. Kwingineko, mamlaka zinazosimamia vyombo vya habari zimefungia mitandao ya habari au kuondoa makala za mtandaoni zinazokosoa serikalil.

5. Kuwatishia na kuwashambulia wanahabari, mtandaoni na nje ya mtandao

Maafisa wa serikali na raia wa kawaida wamejibu ripoti za uokosoaji kuhusu hatua waliochukua kukabiliana na janga hili kwa hasira na vitisho. Katika maeneo ambapo mazingira ya uanahabari tayari yalikuwa hatari, hali imekuwa hatari zaidi.

6. Mahitaji ya kupata kibali na kupunguzwa kwa uhuru wa kusafiri

Mamlaka zimepunguza uwezo wa wanahabari kusafiri na kutembea kwa njia huru, kwa mfano wanapotaka kuripoti wakati wa amri ya kutotoka nje, au kuingia hospitalini kupata taarifa za moja kwa moja kuhusu huduma hospitalini. Wakati mwingine wanahabari wanapewa vibali maalum, lakini kuwahitaji wanahabari kuwa na vitambulisho vinavyotolewa na serikali kunawaruhusu viongozi kuamua ni nani ataruhusiwa kuhudumu kama mwanahabari.

Utafiti wa unaonyesha kwamba hii inaacha wazi uwezekano wa kuwazuia wale wasiofanyia kazi mashirika makubwa ya habari au wale wanaokosoa watawala.

7. Kuzuia kufikiwa kwa habari

Sheria kuhusu uhuru wa kupata habari zinazoruhusu wanahabari kuitisha data, taarifa na stakabadhi za serikali zimesimamishwa. Mikutano na hafla ya kiserikali ambazo wanahabari huhudhuria zimehamishiwa mtandaoni, ambapo kuna viwango mbalimbali vya kuruhusiwa kwa wanahabari kushuhudia au kupata habari. Nchini Marekani, uhasama wa Trump dhidi ya wanahabari unatoa mfano mbaya kwa maafisa wa serikali za majimbo na mitaa.

Gaio aliambia CPJ kwamba mitindo hii huenda ikaendelea. “[Serikali] zitaifanya kuwa vigumu kwa maafisa kutoa habari. Kufikiwa kwa habari kutachukua muda, na itakuwa pia vigumu kwa wanahabari kufika au kufikia maeneo ya umma kutokana na hatari ya kuambukizwa,” alisema.

8. Kufurushwa na kunyimwa viza

Ili kudhibiti taarifa kuhusu hatua zinazochukuliwa na serikali kuhusu COVID-19, baadhi ya mataifa yameanza kutowavumilia wanahabari wa mashirika ya nje, ambao katika baadhi ya mataifa kwa kawaida wamekuwa na uhuru wa kuripoti taarifa zinazokosoa serikali kuliko wanahabari wa mashirika wenyenji.

9. Upelelezi na kuwafuatilia watu

Serikali katika nchi mbalimbali duniani zinafuatilia data za simu kuhusu walipo na wanakoenda watu na pia zinafanyia majaribio au kuanza kutumia program tumishi mpya za kuwafuatilia watu za kutumiwa kufuatilia usambaaji wa COVID-19, kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari. Upelelezi na ufuatiliaji huu unaweza kuwa tishio kwa usiri wa wanaotoa habari kwa wanahabari. Mifumo inaanza kutekelezwa bila uangalizi na usimamizi wa kutosha, na huenda ikaendelea kutumika muda mrefu baada ya janga hili kumalizika.

 “Kumekuwepo na wasiwasi kwamba hali za dharura hutengeneza vipimo vipya vya matarajio ya viwango vya ufuatiliaji wa watu ambavyo serikali zinaruhusiwa kuufanya. Bila shaka tulishuhudia hili likitokea baada ya 9-11, lakini nafikiri suala hilo linajitokeza sasa pia,” anasema  Carrie DeCell, mwanasheria katika taasisi ya kutetea uhuru wa kujieleza Knight First Amendment Institute jijini New York. “Vitendo ambavyo vinaweza kukubalika katika hali kama hiyo havifai kukubalika baada ya serikali kudhibiti janga hili na baada ya janga hili kufifia siku zijazo.”

David Maass, mtafiti mchunguzi wa ngazi ya juu katika wakfu wa Electronic Frontier Foundation wenye makao yake San Francisco, anakubali kwamba kila vyombo vya utekelezaji wa sheria vinapokabidhiwa teknolojia mpya, huwa vigumu kuvipokonya. “Tumeona kwamba sasa wanaitumia kwa sababu ya kukabiliana na virusi hivi hatari,  lakini hatujui kitakachotokea baadaye.”

10. Hatua za Hali ya Dharura

Watawala wa kiimla wanaweza kuchukua nafasi kujifaidi wenyewe kupitia hatua za hali ya dharura ambazo zinaharamisha au kuweka masharti ya watu kukusanyika, kama ambavyo CPJ imenakili awali. 

Huku mataifa mengi yakiwa bado yako chini ya hali ya dharura inayowapa watawala nguvu nyingi za kutawala kwa amri – na virusi hivi ikiwa ndio tu vinaanza kuathiri zaidi mataifa yanayoendelea – kuna uwezekano masharti na vizingiti zaidi vikawa njiani.

Exit mobile version